UBUNIFU NA UADILIFU UTEKELEZAJI MIRADI YA POLISI JAMII!
Kamishna wa Polisi Jamii (CP) Alex Mkama amewataka askari wanaotekeleza majukumu ya Polisi Jamii kwenda sambamba na mabadiliko ya wakati kwa kutumia mbinu bunifu zitakazosaidia kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika jamii.
CP Mkama ametoa wito huo wakati akizungumza na Polisi Kata kutoka wilaya za Kishapu na Shinyanga, Askari wa Dawati la Jinsia na Watoto pamoja na askari kutoka vikosi mbalimbali katika ukumbi wa Bwalo la Polisi Manispaa ya Shinyanga.
CP Mkama, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha utekelezaji wa miradi ya Polisi Jamii kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya wananchi ili kuongeza ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii katika kudumisha amani na usalama.
Aidha, amewahimiza askari hao kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kuzingatia misingi ya taaluma, uadilifu na uwajibikaji, huku akisisitiza mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa vinavyoweza kudhoofisha imani ya wananchi kwa Jeshi la Polisi.
Vilevile, ameeleza kuwa ni muhimu kwa askari kutambua vihatarishi vinavyoweza kuathiri usalama wa jamii mapema, ikiwemo migogoro ya kijamii, ukatili wa kijinsia, uhalifu wa watoto pamoja na matishio mengine ya kiusalama, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa wakati

kwa ujumla, CP Alex Mkama amewahimiza askari kuzingatia ubunifu, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa miradi ya Polisi Jamii ili kuimarisha usalama, kujenga imani kwa wananchi na kudumisha amani katika jamii. .






Maoni
Chapisha Maoni