TPF-NET: WANAWAKE 400 WANUFAIKA NA ELIMU YA UKATILI WA KIJINSIA SHINYANGA
Hii ni Thadeo Media
Leo March 06, 2026 Kaimu Mwenyekiti wa Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania (TPF-NET) Mkoa wa Shinyanga, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Fatuma Mtarimbo, ameongoza Maafisa Wakaguzi pamoja na askari wa vyeo mbalimbali kutoa elimu kwa jamii katika Kata ya Mondo, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Zoezi hilo limefanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambayo kilele chake kitaadhimishwa tarehe 8 Machi 2026, huku maadhimisho ya kimkoa yakitarajiwa kufanyika katika Halmashauri ya Ushetu, mkoani Shinyanga.
Katika mpango huo, wanawake zaidi ya 400 wamenufaika na elimu iliyolenga kuongeza uelewa kuhusu ukatili wa kijinsia, pamoja na kuhimiza jamii kuhakikisha watoto wanapatiwa haki zao za msingi ikiwemo haki ya kupata elimu.
Aidha, Mkuu wa TPF-NET Wilaya ya Kahama, Mrakibu wa Polisi (SP) Flora Nangawe, amewahasa wazazi kuacha tabia ya kupakiza watoto wa shule kwa idadi kubwa kwenye vyombo vya usafiri, wakati mwingine zaidi ya watoto 10 kwa pamoja, akieleza kuwa kitendo hicho ni hatari na ni aina ya ukatili dhidi ya watoto.
Sambamba na utoaji wa elimu hiyo, askari hao wa Polisi Wanawake pia walifanya matendo ya huruma kwa kusaidia familia zenye uhitaji katika eneo hilo, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano na jamii na kuonesha mshikamano katika kipindi hiki cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.
| Kwa ujumla, Hatua hiyo ya TPF-NET inalenga kuongeza uelewa wa jamii kuhusu kupinga ukatili wa kijinsia, kulinda haki za watoto na kuimarisha ushirikiano kati ya polisi na wananchi kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani. |











Maoni
Chapisha Maoni