Wananchi Wa Jimbo JIpya la Itwangi Wajitokeza kwa wingi Kumuunga Mkono Ng. Azza Hillal
Itwangi, Shinyanga – Septemba 13, 2025:
Maelfu ya wananchi wa Jimbo la Itwangi wamejitokeza leo kwenye uzinduzi wa kampeni za Uchaguzi Mkuu, wakionesha kundi la imani na mahaba kwa Mgombea Ubunge wa CCM, Mhe. Azza Hillal Hamad, na kuahidi kumpa kura za ushindi Oktoba 29.
Uzinduzi huo umehudhuriwa na wanachama wa CCM, wagombea udiwani, na viongozi wa ngazi mbalimbali, huku Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (MNEC), Munde Tambwe Abdalla, akiwa mgeni rasmi. Munde alimsifu Azza kuwa “Mbunge Jembe” mwenye ujasiri, uelewa wa masuala ya wananchi na uwezo wa kuleta maendeleo.
Akizungumza na wananchi, Azza Hillal Hamad aliahidi kupeleka miradi ya maendeleo kwenye sekta za maji, elimu, afya na umwagiliaji, akisisitiza kukamilisha skimu za Nyida na miradi ya maji ya Ziwa Victoria na Tinde Package. Pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo SGR, barabara, elimu na afya.
Viongozi wa CCM wakiwemo Katibu wa CCM Mkoa Odilia Batimayo na Mwenyekiti wa Wilaya Edward Ngelela walimsifu Azza kama kiongozi mchapakazi na mnayemuamini. Mbunge Mteule wa Viti Maalum Christina Mzamva aliwahimiza wananchi kumpa kura Azza, Rais Dkt. Samia na wagombea udiwani wa CCM.
Uchaguzi Mkuu unatarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025, ambapo Watanzania watachagua madiwani, wabunge na Rais.
Maoni
Chapisha Maoni