Siasa
Kura za Maoni CCM Itwangi: Azza Hillal Atikisa, Aliibuka Kidedea
Na Mwandishi Wetu – Thadeo Gelema , Agosti 5
Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Mbunge wa zamani wa Viti Maalum Mkoa wa Shinyanga, Azza Hillal Hamad, aliibuka kidedea na atikisa kura za maoni za CCM zilizofanyika jana, tarehe 4 Agosti 2025, katika Wilaya ya Shinyanga Vijijini, kwa nafasi ya ubunge wa Jimbo jipya la Itwangi.
Katika kura hizo za maoni, Azza alipata kura 2,630 kati ya kura 5,580 zilizopigwa, huku kura halali zikiwa 5,551 na kura zilizoharibika 29.
Azza aliwashinda wapinzani wake saba, huku John Elias Ntalimbo akiwa wa pili kwa kupata kura 2,322. Wagombea wengine ni Sebastian Pastory Malunde (kura 377), Fred Romanus Sanga (122), Chrispine Myeke Simon (45), Christian Misobi Budoya (28), Anna James Ng’wagi (16), na Hellena Daudi Mbuli (11).
Katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga Vijijini na Mkurugenzi wa Uchaguzi, Erenestina Richard, alisema kuwa matokeo hayo ni ya awali na siyo uteuzi rasmi.
“Kuongoza katika kura za maoni siyo ushindi wala siyo uteuzi rasmi. Tunawaomba wagombea wote kuwa watulivu na kusubiri maamuzi ya vikao vya juu vya chama,” alisema.
Jimbo la Itwangi ni miongoni mwa majimbo mapya yaliyoanzishwa kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025, likiwa limevutia wananchi na wanachama wa CCM mkoani Shinyanga.
Endelea kufuatilia Thadeo Media kwa taarifa zaidi na za kina.
Maoni
Chapisha Maoni